Mkuu wa Wilaya ya Karatu Mhe. Dkt. Lameck Karanga amekabidhi hundi yenye thamani ya Shilingi Milioni 300 kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye mahitaji maalumu katika hafla iliyofanyika wilayani humo. Fedha hizo ni mikopo ya asilimia 10 inayotokana na mapato ya ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Karatu kwa lengo la kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia shughuli mbalimbali za uzalishaji na biashara.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mhe. Dkt. Karanga amesema serikali inaendelea kuweka mazingira bora ya kuwawezesha wananchi kujikwamua kiuchumi kwa kutoa mikopo isiyo na riba kwa vikundi vinavyokidhi vigezo. Amesisitiza wanufaika kutumia fedha hizo kwa malengo yaliyokusudiwa ili ziweze kuleta matokeo chanya kwa maendeleo yao binafsi na jamii kwa ujumla.
Aidha, amevitaka vikundi vilivyopokea mikopo hiyo kuhakikisha vinarejesha fedha kwa wakati ili kutoa nafasi kwa vikundi vingine kunufaika na mpango huo.
Pia amepongeza Halmashauri ya Wilaya ya Karatu Chini ya Mkurugenzi Juma Hokororo kwa kuendelea kutenga na kusimamia vizuri fedha za mikopo kwa makundi maalumu kwa mujibu wa maelekezo ya serikali.

Post a Comment