Watendaji wa Dawati la Jinsia na Watoto toka Wilaya zote Mkoani Ruvuma wametakiwa kuongeza ufanisi zaidi katika utekelezaji wa majukumu yao kwa kushirikiana na Wadau wengine katika mapambano dhidi ya vitendo vya Ukatili na Unyanyasaji wa Kijinsia ili kuhakikisha tunatokomeza vitendo hivyo katika jamii.
Wito huo umetolewa Aprili 30,2026 na Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto Mkoa wa Ruvuma Mrakibu Msaidizi wa Polisi (ASP) Odiria Mroso katika kikao kazi cha Watendaji wote wa Dawati hilo chenye lengo la kujadili mambo mbalimbali ya kiutendaji pamoja na kufanya tathmini ya utendaji kazi kwa kipindi cha robo mwaka kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Polisi Mkoa Ruvuma.
Akifungua kikao hicho Afisa Mnadhimu namba moja Mkoa wa Ruvuma (SO1) Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Alfred Hussein amewasistiza watendaji hao kuendelea kufanya kazi kwa weledi kwa kutoa huduma bora Kwa wahanga wa vitendo vya Ukatili na Unyanyasaji wa Kijinsia na wananchi kiujumla ili kuhakikisha haki inapatikana na wahusika wanachukuliwa hatua stahiki za kisheria.
Kwa upande wake Mkuu wa Polisi Jamii Mkoa wa Ruvuma Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Ramia Mganga amewaasa watendaji hao kujikita zaidi katika kutoa elimu kuhusiana na mapambano dhidi ya vitendo vya Ukatili na Unyanyasaji wa Kijinsia kwa wananchi ili waweze kupata uwezo na uelewa kuhusiana na vitendo hivyo pamoja na namna ya kuepuka sambamba na kutokomeza vitendo hivyo wahakikishe wanayafikia makundi yote katika jamii.


Post a Comment